watakaoteuliwa kuwa wajumbe wa Kamati Kuu,
MWENYEKITI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais Jakaya Kikwete, amezima
ubashiri juu ya watakaoteuliwa kuwa wajumbe wa Kamati Kuu, ambao majina yao yanatarajiwa kuwekwa
hadharani leo.
Akizungumza wakati akifungua semina kwa wajumbe wa Halmashauri Kuu ya
Taifa (NEC) ya CCM, Rais Kikwete alisema hadi jana hapakuwa na orodha yoyote
iliyokuwa imeandaliwa ya wajumbe hao. Alihoji mantiki ya kauli za ‘kampeni’
kwamba baadhi ya watu wanafaa kuwa wajumbe wa Kamati Kuu ya CCM na wengine ni
hatari na kutaka mambo hayo yaachwe mara moja.
“Nimesikia (wanaosema) hawa ni ndiyo wanaofaa sana,
hawa ni hatari sana,
imekuwaje wajumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa wawe hatari kwa chama chetu?
Jamani acheni,” alisema na kushangiliwa. Alikemea ‘magenge’ hususani wanaotaka
watu wengine waharibikiwe na kusema wanajipa kihoro, hasa pale watakapokuta
hawakuharibikiwa.
Katika semina hiyo ambayo mada mbalimbali zitatolewa na makada na
viongozi wa ngazi ya juu ya chama, Kikwete alisisitiza kwamba watakaowaambia
wanayo orodha ya majina, wanawapotezea wakati. “Napenda niwatahadharishe,
asiwadanganyeni mtu kwamba orodha ndiyo hii; hawa ndio watakaochaguliwa,
anapoteza wakati,” alisema Kikwete.
Kikwete ambaye kauli zake ziliendelea kusababisha vicheko na
kushangiliwa, alisema yeye na Makamu wake wanakaa leo kwa ajili ya maandalizi
hayo. “Tutakaa kesho (leo) wala msiamke usiku huu (jana) mkasema nimekaa na
orodha,” alisema. Msisumbuke kufanya mikutano, kwamba lazima tumuunge mkono
fulani, orodha hiyo haina fulani kwa sababu orodha yenyewe haipo,” alisema.
Aliwataka wajumbe wa NEC walioingia kwa mara ya kwanza kujihadhari na
magenge. Aliwataka wajishirikishe kwenye mambo ya kujenga na wasikubali
kushirikishwa kwenye mambo ya kubomoa. “Kutengeneza magenge mahali fulani huyu
aharibikiwe, ni jambo ambalo halina tija.
Unajipa kihoro hasa pale inapofikia kwamba uliyetaka aharibikiwe
hakuharibikiwa. “Kwa nini ufanye biashara isiyo na maana? Wekeza kwenye kitu
chenye maana badala ya kuwekeza kwenye magenge… Lakini akili ni nywele kila mtu
ana zake,” alisema.
Katika taarifa yake, Katibu wa NEC, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye,
alisema yatatangazwa majina 28 na wajumbe wanaopaswa kuchaguliwa ni 14. Kati ya
hao 14, saba watatoka Zanzibar
na mengine saba watatoka Tanzania Bara. Alisema watazingatia pia jinsia katika
uchaguzi wa wajumbe hao.
Maadili
Miongoni mwa mada zilizotolewa jana katika semina hiyo ni suala zima la
maadili, ambalo Kikwete alisema kiongozi anapaswa kuwa na maadili mema kwa kuwa
ndiyo taswira ya chama. Alitoa mfano kwamba ikitokea mjumbe wa NEC akawa mlevi,
chama pia kitaonekana ni cha walevi. “Mjumbe wa NEC unalewa, wewe ndiye wa
mwisho kuondoka baa, unamalizia kwa kusema kidumu Chama Cha Mapinduzi, watu
wataona chama cha walevi,” alisema.
Alisema haiwezekani mjumbe wa NEC akawa mtu wa kukopa mara kwa mara
kiasi cha kusababisha anapopigia watu simu wanaikataa wakijua atakopa.
Ajira
Alisema ajira ni tatizo lakini haitoshi kuzungumzia bila kutoa jawabu
lake. Alisema haipaswi mtu kulaumu bila kutoa njia mbadala ya kumaliza tatizo.
Aliongeza kuwa ingawa suala la kutoa ajira siyo la moja kwa moja ndani
ya CCM, wameamua lijadiliwe kwa kuzingatia ndicho chama tawala kinachoweza
kuelekeza Serikali nini kifanyike. Hata hivyo, alisisitiza kwamba suala la
ajira si la Serikali pekee bali pia la sekta binafsi.
Alisema katika Serikali wigo wa nafasi za ajira ni ndogo,
ikilinganishwa na sekta binafsi. Hata hivyo alihoji: “Ni namna gani sekta
binafsi itatoa ajira wakati wawekezaji wakiendelea kuitwa wezi na wakati huo
huo wanaowekeza wakifanyiwa fujo wasiwekeze?”
Maazimio
Akielezea mkakati wa kutekeleza maazimio ya Mkutano Mkuu wa Taifa wa
Novemba mwaka jana, Kikwete alisisitiza lazima yatekelezwe kwa kuwa heshima ipo
kwenye kutekeleza wanayotamka. Alisema watajipanga vizuri namna ya
kuyafanikisha.
No comments:
Post a Comment