Friday, June 21, 2013

MWENGE WA UHURU WILAYANI YA ARUSHA.

Mkuu wa Mkoa wa Arusha,Magesa Mulongo(kulia)akimkabidhi Mkuu wa wilaya ya Karatu Mwenge wa Uhuru ukimbizwe wilayani humo


Sote tunatambua kwamba kihistoria, mwenge wa Uhuru uliwashwa ili kuleta matumaini pasipo na matumaini, kuleta upendo palipo na chuki, na heshima pale ambapo pamejaa dharau. Hadi sasa, pamoja na kuhimiza maendeleo kwa wananchi, Mwenge wa Uhuru bado unabeba maana na madhumuni yale yale yaliyoainishwa wakati unawashwa.

Katika mwaka 2013 Halmashauri ya Jiji la Arusha  imepokea Mwenge wa ishirini na moja (21) tangu Mwenge wa Uhuru ulipowekwa chini ya utaratibu na usimamizi wa Serikali mwaka 1992. 

Mwenge wa Uhuru katika Jiji la Arusha ulipokelewa  tarehe 07 Juni, 2013 kwenye Kata ya Olasit, eneo la uwanja wa Kiwanda cha A-Z- Kisongo na ulikimbizwa kwa siku moja katika Tarafa tatu (3) za Themi, Suye na Elerai. Aidha mwenge ulipita  katika Kata sita (6) kati ya kata kumi na tisa (19) za Wilaya hii. Kata hizo ni Olasiti, Sombetini, Terrati, Sokoni 1, Engutoto na Sekei. Mbio za mwenge wa Uhuru za Mwaka 2013 zimekuwa  na urefu wa kilometa 71.25 katika Wilaya ya Arusha. 

Jumla ya miradi 8 ya maendeleo yenye thamani ya Shilingi Billioni mbili, millioni mia nane na mbili  laki moja na themanini na mbili elfu mia saba na saba (2,802,182,707/=) ambayo imegharamiwa na Serikali Kuu, Wabia wa Maendeleo, Halmashauri, na nguvu za Wananchi imepitiwa na Mwenge. Miradi minne (4) imefunguliwa, mmoja (1) umezinduliwa na mitatu (3) imewekwa mawe ya msingi.

Miradi yote iliyopitiwa na Mwenge imegusa Sekta za Kilimo, Maji, Afya, Ujenzi, Elimu na Utawala bora. 

Aidha, Mwenge ukiwa Jijini Arusha ulikagua miradi ya Uhifadhi wa Mazingira, masuala ya kupambana na Rushwa, Ukimwi, Madawa ya kulevya na shughuli za Ujasiriamali kwa Vijana na Wanawake.

Hakika miradi hii yote  inastahili kufunguliwa na Mwenge kwa sababu ya umuhimu wake kwa jamii ya wananchi wa Wilaya ya Arusha. Miradi yote iko katika hatua nzuri na thamani ya fedha inaonekana.

Mkuu wa Wilaya ya Arusha Mhe. John V.K. Mongella akizungumzia tathmini ya miradi iliyofunguliwa na Mwenge alisema “ Kupitia miradi yote iliyopitiwa na Mwenge wa Uhuru 2013, Wilaya yetu imeweza kuandaa fursa ya nafasi kwa wanafunzi wanaomaliza darasa la Saba waweze kujiunga na masomo ya Sekondari kupitia Ujenzi wa madarasa, kurahisisha usafiri kwa wananchi katika  uboreshaji wa Miundombinu, kuongeza Upatikanaji wa huduma za Afya kwa Kwa kujenga Zahanati, kusambaza maji safi na salama kwa wananchi, kuimarisha Usalama wa Raia na kupunguza Uhalifu kwa kujenga Kituo cha Polisi na Utunzaji wa mazingira.

Aidha Mkuu wa Wilaya amewashukuru wadau mbalimbali waliohusika kwa namna moja au nyingine katika kuibua, kuchangia na kufanikisha miradi yote iliyopitiwa na Mwenge. Pia wananchi wote wa Wilaya ya Arusha waliojitokeza kwa wingi kupokea, kukimbiza na Kukesha na Mwenge.

Ujumbe wa mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka huu utakimbizwa ukiwa unaelimisha na kueneza ujumbe wa ‘‘Watanzania ni wamoja’’ chini ya kauli mbiu ‘‘Tusigawanywe kwa misingi ya tofauti zetu za Dini, Itikadi, Rangi na Rasilimali’’ Aidha ujumbe huu umeambatana na kauli mbiu ya Miaka 50 ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar ni Ushindi wa Watanzania wote na mapambano dhidi ya UKIMWI, Rushwa na  matumizi ya dawa za kulevya.

Mwenge wa Uhuru mwaka huu uliwashwa tarehe 06 Mei, 2013 huko Mkoa wa Kusini Pemba na utazimwa tarehe 14 Oktoba, 2013. Mkoani Iringa.

Nteghenjwa Hosseah

Afisa Habari

Halmashauri ya Jiji - Arusha


No comments:

Post a Comment

 
Support : Katibu Mwenezi CCM (w) Arusha | Jasper Kishumbua | CCM Arusha
Copyright © 2011. CCM Dijitali Blog - Arusha - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by Jasper Kishumbua
Proudly powered by Blogger